Showing posts with label Menu ya Kitaani. Show all posts
Showing posts with label Menu ya Kitaani. Show all posts

Friday, July 11

Tuanze wikiendi nyingine pamoja

  Wikiendi si ndo inaanza, leo sisemi sana nakujuza kuwa iwapo utataka kupata menu hiyo hapo ambayo ni samaki walipikwa na viepe ndani ya foili, basi ifwate Shikamoo pesa bar iliyopo Sinza kwa wajanja.
  Zaidi ya menu hiyo, kuna biriani, kokoto, mbuzi katoliki toka kwa jirani, mihogo ya kukaanga na chachandu yake na mengineyo mengi huku ukishushia na vinywaji mbalimbali bariiiidi na muziki murua. 
 Kaka Fredy anasema, Karibuni

Thursday, July 10

Wikiendi ndefu na menu zake

  bado twaendelea kukujuza yalojiri katika hii long wikiendi ambapo ilianza Ijumaa hadi Jumatatu ambapo tulikua tunatimilisha sikukuu ya wakulima hapa tanzania.
  sasa siku ya Jumapili, tulipata kwenda kuosha macho viwanja vya sabasaba nikiwa na mama yangu, na baada yakutoka hapo na kufaidi mengi, tukaona tupite mgahawa mmoja katikati ya mji ujulikanao kama Mokka City lounge na menu tuliyoipata ni hii hapa chini...... karibuni
  Mimi kama kawaida yangu nilipata menu hii ambapo ipo hivi, ni vimikate vya pizza ambavyo ndani kuna vipande vya nyama ya kuku na viungo vingine, huku ikisindikizwa na salad pamoja na mayonnaise

Mama yeye alipata kujaribisha biriani ya kuku, na moja ya neno alitoa ni kwamba biriani hii ilikosa lile rojo la kibiriani ambalo walipata kitaani au mtu akilipika home, Uzuri mwisho wa siku alipata kuenjoy jinsi ilivyo maana upishi watofautiana, na ilikua ni vyema kujaribu mapishi mengine.

   Fanya kuwapitia hawa Mokka City lounge waliopo mjini katikati iwapo mida ya menu itakupata eneo hilo, au iwapo wataka kujaribisha mapishi ya aina tofauti.
   kutoka kwetu, kutoka wikiendi ndefu ndo tunakomea hapa na tutarejea kesho tuanze kuangalia wikiendi hii twaanzia wapi. Karibu kutujuza wapi mtakuwepo wewe na marafiki zako kupitia anwani yetu menutimes@gmail.com

Friday, June 20

Masai Club - Mwananyamala

  Ijumaa ndio hii, enhee tujuzane mapemaaaaaa..... leo mtoko wapi, haya kama utabaki nyumbani menu gani watayarisha, na je utakula na nani?
  Wiki iliyotangulia, siku kama ya leo tulipata kufika pande za Mwananyamala, ilipo Masai bar ambapo huko kuna kila aina ya starehe uitakayo. Kuanzia vinywaji, muziki, vyakula na mengineyo.
  Moja ya menu tuliyopishana nayo ni supu ya ng'ombe na ushuhuda ni huo hapo chini. Imesindikizwa na mbogamboga ndani ya supu, kuna ndizi humu na kwa pembeni ndimu na chumvi vya kunogesha mambo

   Kutokana na kwamba sio Rafiqs wote walipendezwa na kupata supu mida ile, basi wao waliamua kuagizia mishkaki, kiukweli ni milaini na mitamu sana sana. Pongezi kwa bwana mpishi.
   Mambo ni mengi yanatokea siku ya leo, karibu kushare nasi yatakayojiri pande ulizopo. Anwani ni menutimes@gmail.com au tufwate kwa social medias... instragram tupo @menutimes na kwenye kitabu sura a.k.a facebook, page yetu ni www.facebook/Menutime.com na kwa twitter ni @menutimetz
  Haya tukutane huko kwa habari zaidi za kiwikiendi.

Thursday, June 19

Kinondoni

   Leo tupo Kinondoni, na ndo mambo ya wikiendi yanaanza na si wote twajua starehe zote zipo Kinondoni, basi mapema tujuzane menu ipi unapata wapi kwa nani  na mengineyo, sababu tunaijua ni kupata utamu
  Sasa pale Hugo Kinondoni wafanya kama wakata kona waelekea palipo baa maarufu sana kinondoni, mkono wako wa kushoto, utaona kontena pale ambapo mambo haya ndo yapatikana. 
Tulipishana na biriana moja matata sana, ambapo ilisindikizwa na tunda la ndizi pamoja na Fanta baridii.

  Kwa pembeni pale alipo Rafiq yetu wa kitambo, bado anafanya mabo yake na ile nyama yetu ilee. Cha leo kilikua cha makange na muonekano wake ni kama huo khapo

  Tunaendalea kujitayarisha na kukutayarisha wewe na wikiendi, na kwa kumalizia tunaenda kuleeeee Masai club mitaa ya Mwananyamala. Hawalali Rafiqs wa pande zile.

Wednesday, June 18

Posta, upanga na mambo ya Miksii

  Na kwa kuwakaribisha posta, tulimaanisha pande za Upanga ambapo kuna sehemu wako makini katika upikaji na utengenezaji wa bajia, kababu na miksii ambapo ukianza kwenda hapo hutoacha.
   Muda wa kufunguliwa na mauzo kuanza ni saa kumi na moja jioni pale ambapo wengi tumetoka maofisini, twaelekea makwetu, na huwepo hadi kwenye saa tatu usiku.
  Karibu kuona menu tulizozipata pale tulipowatembelea Rafiqs hawa.
   Tunaanza na miksi ambapo ni mchanganyiko wa mambo mengi matamu na kwa pamoja muonekano wake huwa hivi

  Wengine hawakupenda miksi, bali walitaka wapate bajia au kachori na wanauza sh 2,000 kwa sahani ambapo wasindikizwa na chetna iliyo na kila aina ya utamu, na pilipili kwa pembeni kama utapendelea.

 Kwa ukaribu zaidi na upendeleo
   Tunahama kutoka Upanga, a.k.a Uhindini hadi Kinondoni, na ifikapo kesho ntawajuza yaojiri kinondoni

Friday, June 13

Twamalizia Chang'ombe

   Ikiwa imetimu ijumaa, tunaondoka pande za Chang'ombe yaani pale tulipokua tumefunga kambi kwa siku tatu zilizopita, naongelea TCC Club.
   Tukapishana na aina ingine ya menu ambapo nilikua naitegea sana, naongelea dagaa.
hapa tuna wali mweupe, mbogamboga kama kisamvu, majani ya maboga na spinch pamoja na dagaa

  Twakutakieni mapumziko mema ya mwisho wa wiki, na karibu kutujuza wapi twapumzika, na je ni menu ipi tunapanga kupika/ kupata na wapi.
   Wasiliana nasi kwa kutuma picha za menu zako mbalimbali kupitia menutimes@gmail.com

Thursday, June 12

Bado tupo TCC Chang'ombe

   Bado tupo Chang'ombe na twaendelea kutaste menu zao. Suala la kurejea hapa na kuendelea na zoezi la kupata menu ni alama tosha kuwa wana menu nzuri na tamu na yafaa kufwata tena na tena ili kuenjoy mengineyo ambayo hatukuyapata juzi.
  Basi jana mlo tulioupata pale ni huu hapa

  Hapo kuna ugali, nyama ya ng'ombe iliyochanganywa wakati wa upikwaji na mchicha na pembeni kuan majani ya maboga. lakini mlo huu una jina lake spesheli ufikapo pale na kama wataka kuupata. wajulikana kama ..........
   Twawatakia kila la kheri katika Alhamisi hii njema.

Wednesday, June 11

Mambo ya TCC Chang'ombe Club

    Katika pitapita zetu jana, tulipata kuwatembelea TCC Chang'ombe Club. Eneo kongwe lijulikanalo na maelfu ya watanzania, na nikiwa pale nilipata kujua kwamba ndio club za kwanza za soka nchini Tanzania, na uwanja ule basi ulipatwa kukanyagwa na wanasoka wengi mno, ambao ni mababu zetu, baba zetu, wajomba na hata kaka zetu, na pengine watoto na wajukuu zetu, inategemea tuliopitia na kuujua uwanja huo muda gani.
   Kitu kimoja kuhusu ule uwanja nachopenda sana ni mazingira yake yako tulivu mno na ni sahihi haswa kwa wale wafanyao mazoezi ya viungo katika kujiweka fiti na maisha.
  Pia upande wetu wa maakuli, wapo vizuri ambapo vyafwatana na muda naamini na matukio pia hutofautiana. Mchana siku za juma kwa ujuzi wangu panapikwa vyakula mbalimbali vya kuungwa, kuchoma, kukaangwa na kadhalika, ni wewe tu na maamuzi yako ya siku hiyo.
  Tusiongee sana, jana menu tuliyopata ni hii hapa,
Samaki wa mchuzi alopikwa na pilipili |(ugonjwa wangu).

   Samaki huyo alisindikizwa na mboga ya maharagwe, mboga ya majani pamoja na wali wa nazi ambao ndo ilikua menu yangu. Pembeni kuna vikorombwezo kama kawaida, huku tukishushia na maji safi ya kunywa.
  Kesho tutarejea kuwajuza menu nyingine zinazopatikana pande za TCC Chang'ombe. Tunawatakia siku njema leo.

Tuesday, June 10

Kifungua kinywa

  Asubuhi ya leo tumeamkia mitaa ya Temeke, ambapo tulisimama moja ya eneo la tukio tupate kufungua vinywa vyetu na kwenye ubao wa pale, paliandikwa mambo mengi ila binafsi nilivutiwa na supu ya mbuzi na baada ya kuiagiza, muonekano ulikua namna hii
    
   Kiukweli supu ilikua tamu na ya motooo, kwahiyo kama utamu unazidi vilee. Pembeni kama kawa kuna vikorombwezo visindikizavyo mpango mzima nawaongelea wakina ndimu, pilipili, chumvi na wenzie.
   Je, Jumanne hii mmefungua vipi kinywa Rafiqs??

Monday, June 9

Menu ya leo

Nikiwa na Rafiqs pande za Chang'ombe tumepata menu hii mchana huu.


                                   
   Kuna chapati, maharagwe, nyama na mbogamboga.
Karibuni!!!

Tuesday, May 27

Mchana twaupitishaje????

    Mchana wetu tumeanza taratiiibu kwa kula menu ambayo hatutashiba sana. Tupo nyumbani hapa.
    So tumeanza na mtori


 
     Kisha tukapata salad.
                            
 
Tujuze wewe umeupitishaje wa kwako? Na wapi upo?

Tuesday, April 1

Mihogo ya Coco Beach

   Tulipata wasaa wa kupita maeneo ya ufukweni, mjini Dar es salaam, tunaongelea Coco  
beach, ambapo ni maarufu sana kwa upepo mwanana, kuogelea na menu mbalimbali zipikwazo pande hiyo.
  Kunakuwa na mix, mishkaki, mihogo, viazi vilivyokaangwa pamoja na vipande vyembamba vya aidha viazi au mihogo vilivyokaangwa na kutengeneza crisps.
   Sisi tulipata kula crisps, mhogo na kiazi cha kukaanga vikisindikizwa na chachandu, kama picha ioneshavyo hapo chini

   Ukipata wasaa wa kupita Coco beach, je ni menu gani hupenda kuipata?

Wednesday, March 26

Menu ya Woodmont & T.Bonaz

Kutoka pande za Ali Hassan Mwinyi road, kuna kijiwe cha kuchill na washkaji kadhaa ambapo marafiqs huwa wanakutana katika kubadilishana mawazo. Paitwa Woodmont & T.Bonaz na wajulikana kwa utengenezaji wa menu tamu na safi.
  Moja ya menu tuliyokutana nayo ni hii hapa, vibawa vya kuku na vipande vya viazi vya kusindikizia na salad na vikorombwezo kadhaa.

 
    Fanya kupita hapo, na upate kuonja menu yao. 
Twawashukuru sana kwa ukarimu wao, wana  Woodmont & T.Bonaz.

Tuesday, March 25

Kachori na bajia

  Kuna baadhi ya vyakula hupenda kuviita vyakula vya hamu, yaani unajikuta umekamatwa na hamu ya kupata ladha flani, basi utatoka kuitafuta hiyo menu.
  Ugonjwa huo upo katika bajia na kachori zipikwazo mitaa ya Upanga, ambapo kuna miksi pia. 
  Karibu kuona picha za nayoyaongelea huku vkisindikizwa na chetna
Kachori

  Bajia

  Kikorombwezo chetna
 
   Tuambie wewe wapenda menu gani? au jushikwa na hamu ya menu gani? anwani yetu ni menutimes@gmail.com. Karibu

Thursday, March 13

Ugali dona

  Hivi imewahi kukutokea kwamba kuna menu flani hujawahi kuila toka umezaliwa ilihali inapatikana unapoishi? Aidha inakua wazazi wako hawakukulisha au ni kwamba ulikua hukutani navyo, pengine hukuvipenda au wazazi hawakuvipenda au hawakuvitilia maanani, maana tuwapo wadogo, maamzi ya leo kipikwe nini yapo mikononi mwa wazazi mpaka pale nasi tunapokuwa na kwetu na maamuzi yetu ya leo tunakula, hatuli na kama twala basi twala nini yanakuwa ni juu yetu ni si wazazi wetu tena!
  Mmoja wa wana Menu Time hakuwahi kula mlenda hadi hivi juzi alipopishana nao sehemu na kuanza kuugida kwa pupa.
  Maelezo yake ni kwamba una ladha ya ajabu yani ya pekee na alipoujaribu, aliula kwa siku nne mfululizo bila kuuchoka huku akisindikiza na ugali,  samaki alioungwa na tui la nazi na mboga mboga nyinginezo.
  Hapa chini ni ushuda wa moja ya milo yake alipofumania mboga ya mlenda na kuipenda


  Ugali ni ule wa dona, na mboga mboga zilizosindikiza mlenda ni spinach pamoja na keabichi

   Tujuze ni menu ipi umeanza kuila ukubwani kupitia menutimes@gmail.com, pia tufwate instagram kupitia @menutimes kupata kujua yalojiri hapo kwa hapo na team ya Menu Time.
  Twawatakia Alhamisi njema!!

Wednesday, March 12

Ugali mweupe

   Leo twaangallia ugali, mlo wetu wa kitanzania kabisa, wa kinyumbani upendwao na wengi na pia huliwa na wengi huku tukitofautiana kwenye mboga.
   Leo tumekula ugali wa mahindi, dagaa walioungwa kwa nazi na kupikwa na nyanya chungu 
pamoja na mlenda, huku tukishushia na maji safi ya kunywa

       Tujuze wapenda kula ugali na mboda gani? je, wapika mwenyewe au waenda sehemu kula tujuze ni wapi nasi tujumuike.
     Twawatakia Jumatano njema yenye baraka tele.

Friday, March 7

Supu ya Pweza

   Kwa mara ya kwanza tumepishana na supu ya pweza na kuamua kuionja. Pengine pweza alikaa kwenye jokofu mda mrefu, au mpishi alikosea sehemu katika upishi. Pengine ndiyo ladha yake, ila kwa wale muitumiayo mara kwa mara tafadhalini tujuze, ladha ya supu ya pweza ikoje???
  Ushuhuda wa supu tuliyoipata lakini hatukuipenda kwasababu haikua na ladha yoyote

  Chapati ilikua tamu muno, na kwa hilo huku tukisindikizwa na vikorombwezo, supu ilinyweka. 
Tujuzeni ladha ipoje?? tuandikie menutimes@gmail.com

Thursday, February 20

Nyumbani Lounge

Paitwa Nyumbani lounge na wengi  mwapafahamu. Ni lounge ya Lady Jaydee na mumewe bwana Gadner Habash a.k.a Capitain.
   Mara kwa mara huwa twaenda pale na kuna kitu kizuri kitaja fanyika pale kati yetu wana menutime na Nyumbani lounge.
   Baadhi ya supu zinazopatikana pale ni pamoja na ...


  Pia kuna supu ya kuku wa kienyeji, na ushahidi wake ni huu 
  Kujua zaidi yanayopatikana hapo Nyumbani lounge wafwate kwenye instagram, waitwa @nyumbanilounge

Wednesday, February 12

Vegetarian lunch yaani menu isiyo na nyama

  So mchana wa leo tumeamua kula chakula ambacho hakina nyama, yaani kile maalum kwa wasiokula nyama a.k. a vegetarians
   So tukaenda sehemu yaitwa pizzeria katikati ya Rock city na kuagiza pizza isokuwa na nyama
   Ushuhuda wetu ni huu

Imepikwa na mdikodiko mengi, kuna kitunguu swaumu, uyoga na wenzie wengi ikifunikwa na jibini ya kutosha.
Hakika ilikua tamu mno.

Tuesday, February 11

Musoma cha mchana

  Leo tumefika Musoma mjini..... tunashukuru Mungu tunatembelea mikoa mingi hapa Tanzania.
  
 Menu ya mchana ilikua hii hapa

  Kuna ndizi kaanga na kuku wa kienyeji aliyerostiwa. Tukashushia na fanta passion na maji safi bariiidi. Eneo ni Orange tree hotel.
  Tunarejea Mwanza... tutakujuza cha usiku.